Banza Stone aliyezaliwa mwaka 1972 na kufanikiwa kumaliza
elimu ya msingi katika shule ya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam mwaka 1987,
alianza taratibu kujihusisha na masuala ya muziki akiwa angali mdogo.
Banza alianza muziki miaka 25 iliyopita, mara tu baada ya
kumaliza elimu yake ya msingi kwa kujihusisha na muziki wa Hip Hop, enzi hizo
walikuwa wakisikiliza katika redio. Wakati huo alikuwa na wenzake kama kina K
One na Scoz Man.
Wazazi wake waliweka pingamizi baada ya kuonekana muziki huo
kuwa wa kihuni na mwaka 1990 akaamua kuanza mchakato mpya wa kuwa mcheza dansi,
alicheza dansi kwenye maharusi na kufanikiwa kupata fedha kidogo. Banza aliamua
kwenda shule kusomea masuala ya mziki kwenye chuo cha utamaduni cha Korea ,
Korea Cultural Music Centre mwaka 1990 mpaka 1991.
Baada ya kuhitimu cheti alianza kuimba katika bendi mbalimbali
ikiwamo The Heart Strings, Twiga Band, Achigo Band kama mpiga ngoma, Afri-Swez
na bendi nyingine ndogo ndogo. Alikuwa akidumu katika bendi kwa miezi kadhaa,
kabla ya kuhamia katika bendi nyingine mpaka alipoingia katika bendi ya The
African Stars, Twanga Pepeta na kuijenga bendi hiyo barabara.
Alijiunga na chuo cha Sanaa Bagamoyo mwaka 2000 ambapo
alipata mafunzo kwa miaka miwili, alipomaliza alitoka Twanga Pepeta na kwenda
Tanzania One Theatre (TOT) na huko alijulikana zaidi kwa jina la Mwalimu wa Walimu
japo hakukaa sana na kuamua kuanzisha bendi yake iliyokuwa ikiitwa Bambino
Sound ambayo ilidumu kwa miezi kadhaa tu lakini ilivunjika kutokana na kutokuwa
na uongozi mzuri na akarudi African stars Band na baadae kuhamia Extra Bongo.
Katika kipindi cha miaka 23 tangu aanze muziki wa dansi
rasmi haikuwa rahisi kwake kupata mafanikio, kwani alizunguka sana mpaka kuifikia bendi ya The African
Stars Twanga Pepeta mwaka 1995. Banza Stone alipitia zaidi ya bendi tisa
ikiwemo Rufita Band. Mwaka jana msanii wa muziki wa kizazi kipya, Hamisi
Ramadhani H-Baba aliamua kumshirikisha Banza kurekodi wimbo wake mpya wa Sina
Raha.
Banza Stone amewahi kutamba na nyimbo kadhaa zikiwemo: Mtaji
wa Maskini, Kumekucha, Elimu ya Mjinga, Angurumapo Simba Mcheza Nani na Falsafa
ya Maisha. Amewahi pia kuimba vibao kadhaa vya taarabu ukiwamo Kuzaliwa Mjini
na ule wa Play Boy.