F Mwigulu atangaza mamia ya ajira | Muungwana BLOG
https://c2p.cleverwebserver.com/dashboard/6a0bec4b-79ba-11ef-ad2b-06f0639468d1

Mwigulu atangaza mamia ya ajira

Akizungumza jana wakati wa kikao cha kujadili utendaji ndani ya jeshi hilo, Mwigulu alisema katika mwaka wa fedha wa 2017/18, serikali imepanga kuajiri askari wapya 600 ndani ya jeshi hilo ikiwa mkakati wa kupunguza uhaba wa watumishi ndani ya chombo hicho.

Kutangazwa kwa ajira hizo, ni mwendeleo wa serikali katika kuhakikisha inapunguza tatizo la watumishi serikalini ambako kwa sasa kuna uhaba mkubwa kutokana na sababu mbalimbali ikiwamo kuondolewa kwa wale waliobainika kuwa na vyeti feki.

Juzi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, menejimenti ya utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angellah Kairuki, alitangaza ajira mpya 10,000 kwa watumishi wa kada mbalimbali kwa ajili ya kufidia pengo hilo.

Waziri Mwigulu alisema, ndani ya Zimamoto na Uokoaji, serikali imedhamiria kushughulikia masuala ya kisheria, maslahi na yale ya kiutendaji ili kulifanya kuwa na hadhi sawa na majeshi mengine yaliyoko chini ya wizara hiyo.

Akifungua kikao hicho cha siku mbili, alisema serikali inatambua changamoto zinazolikabili jeshi hilo ikiwa ni pamoja na upungufu wa askari na kwamba kwa kuanzia wataanza kuajiri idadi hiyo ya askari.

 Sambamba na hilo, alisema serikali itafanya mabadiliko makubwa katika mambo mbalimbali ndani ya jeshi hilo ili kuendana na hali iliyopo sasa.

“Pelekeni orodha ya mapendekezo ya baadhi ya sheria mnazoona ni mbovu kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa maombi ya kuzibadilisha ili kuondoa mgongano,” alisema Nchemba.

Alibainisha kuwa jeshi hilo limekuwa na changamoto mbalimbali ambazo serikali inatakiwa kuzifanyia kazi ikiwa ni pamoja na maslahi ya askari na mambo mengine ya kiutendaji ambayo yamekuwa yakilalamikiwa.

Kuhusu upungufu wa magari, Waziri Nchemba alikiri kuwapo kwa tatizo hilo hasa magari ya kuzimia moto na magari ya makamanda wa mikoa.

Alisema hiyo inatokana na bajeti inayotengwa kutosheleza kununua magari mawili kila mwaka huku mahitaji yakiwa bado makubwa.

Kwa upande wake, Kamishna Jenerali wa Zimamoto na Uokoaji, Thobias Andengenye, alisema kwa sasa jeshi hilo lina watumishi 2,247 na kwamba idadi hiyo ni ndogo kulinganisha na huduma zinazotolewa.

Alisema upungufu wa askari hao umekwamisha ufunguaji wa ofisi katika wilaya mbalimbali kwa kuwa ikifunguliwa ofisi inabidi kupunguza askari kutoka shifti zilizopangwa na kuwahamishia wilayani.

Andengenye alisema matarajio yao mpaka kufikia mwaka 2030 ni kuwa na askari 25,000 na kuomba kuongezewa wigo wa ajira ili wafikie malengo hayo.