Aliyenunua madiwani ajisalimisha kwa mganga

Mtuhumiwa mmoja aliyeshiriki kununua madiwani wa CHADEMA Meru amejisalimisha kwa mganga wa kienyeji ili kulinda kibarua chake kisiweze kuota nyasi kufuatia uchunguzi mbalimbali ambao unaendelea.

Mbunge wa Jimbo la Arumeri Mashariki, Joshua Nassari amethibitisha hilo na kusema kuwa mtuhumiwa huyo anaishi maeneo ya Mukidoma Usa- River na kudai kuwa tayari anao ukweli wote kuhusu hilo na kuahidi kuutoa muda si mrefu.

"Mmoja wa watuhumiwa wa rushwa ya ununuzi wa madiwani Meru aishie maeneo ya Mukidoma Usa-River ameleta mganga toka kanda ya ziwa, na yupo nyumbani kwake . Lengo ni kumsaidia mtuhumiwa huyu asipoteze ajira yake. Mganga huyu ameletwa na mama wa mtuhumiwa. Tutaanika hadharani acha tuone tofauti ya Mungu na miungu" aliandika Joshua Nassari

Mbunge wa Jimbo la Arumeri Mashariki, Joshua Nassari siku kadhaa zilizopita aliachia ukweli juu ya wateule wa Rais John Pombe Magufuli jinsi ambavyo walikuwa wakipanga mipango ya kununa madiwani wa CHADEMA na baadaye alichukua ushahidi huo na kuupeleka TAKUKURU.