Ramsey Noah atua Bongo, azungumza na wanafunzi wa UDSM


Mwigizaji na mtayarishaji wa filamu wa Nigeria, Ramsey Nouh amewataka vijana wa Tanzania kuwa na shauku ya mafanikio na  kutokubali kurudishwa nyuma katika juhudi za kujikwamua.

Nouah ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Chuo Kikuu  cha Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa mradi wa uhamasishaji na kuwajengea uwezo vijana, kutambua na kusimamia ndoto zao unaoratibiwa na kampuni ya mafuta ya Sahara Group ukilenga kuwafikia zaidi ya vijana 10 milioni.

Nouah ambaye pia ni balozi wa Sahara Group amesema hakuna mafanikio ambayo yanaweza kufikiwa bila kupitia changamoto hivyo ni muhimu kwa vijana kukabiliana nazo bila kuyumbishwa.

Akijitolea mfano amesema mafanikio aliyoyapata hakuja kwa urahisi kwani alipigana na kusimamia alichokuwa akiamini.

“Imani yangu ilikuwa kwenye filamu, nilikuwa na shauku ya kufanya vizuri kwenye tasnia hiyo, sikujali changamoto nilizokutana nazo. Nilisimama na kufanya kazi kwa juhudi zaidi hadi pale watu walipoanza kunielewa,”

Sambamba na Ramsey, wengine waliopata nafasi ya kuzungumza na vijana hao ni mjasiriamali Jokate Mwegelo na mshindi wa Big Brother Africa mwaka 2014 Idris Sultan.

Kwa upande wake Jokate aliwataka vijana kuwa wabunifu na kutumia mawazo katika kuleta mabadiliko na maendeleo kwenye jamii.

“Ni nadra sana ukafanikiwa kwa kuiga kitu cha mwingine. Tujaribu kuwa na ubunifu, nilipomaliza chuo nilipata ufaulu mzuri ulioniwezesha kuendelea kubaki kufundisha chuoni lakini sikutaka nikafungua kampuni ya urembo, wengi walinishangaa wakaniona kama nimechanganyikiwa. Hilo halikunipa shida kwa sababu kichwani mwangu nilijua nini nataka,”