Chege atoboa siri alivyoumia kuvunjika kwa TMK

Msanii Mkongwe kutoka TMK Chege Chigunda amekiri kuwa aliathirika kisaikolojia baada ya kundi la TMK Wanaume Family kuanza kuvunjika.

Chege ametoa kauli hiyo leo na kusema kwamba boss wake ndiye aliyemtia  moyo na kumfanya azidi kupambana na kufikia mahali ambapo anapataka.

Chege amesema kwamba "Nisiwe muongo kuvunjika kwa TMK Family kulinifanya niathirike kisaikolojia. Namshukuru sana Bosi wangu alinitia moyo na kuniambia kwamba nilikuwa pale kwa ajili ya kujitengeneza na siyo kumtegemea mtu aniimbie. Ujasiri wa maneno yale ndiyo yaliyonitia nguvu"

Akizungumzia kuhusu yeye na Temba kuonekana maarufu ndani ya kundi kuliko wasanii wengine, Chege amesema kwamba kwenye kundi hakuwezi kuwa na watu maarufu wawili na kuongeza kwamba ndiyo maana yeye na Temba walibahatika.

Akizungumzia kuhusu wao wawili kuonekana na kusikika zaidi ikiwa ni pamoja na kutengeneza kombinesheni pamoja na Temba, Chege amesema kwamba muunganiko wao ulitengenezwa na wahindi ambao walipenda kazi yao na baadae kuamua kufanya kazi na muunganiko huo wa Chege na Temba.