Anthony Joshua na Joseph Parker nani mbabe

Leo Wales na dunia nzima itasimama kwa muda kuangalia pambano la wanamasumbwi wawili mahiri wa uzito wa juu duniani (heavyweight), Anthony Joshua wa Uingereza na Joseph Parker wa New Zealand.

Pambano hilo la kuwania ubingwa wa Dunia wa uzito wa juu katika mikanda minne ya WBA ,IBF, IBO na WBO , litapigwa uwanja wa Principality Cardiff nchini Wales, uwanja mbao Joshua mwaka jana alitetea mikanda yake dhidi ya Carlos Takam,

Wakali hao wa ndonga wameunganisha mikanda yao Joshua akiweka mezani mikanda yake ya ubingwa wa dunia wa WBA,IBF na IBO huku Parker akiweka mezani mkanda wake wa dunia wa WBO.

Mabondia hao wote ni mabingwa wa dunia na wote  hawajapigwa hata pambano moja, Joshua akiwa na rekodi ya 20-0 akishinda yote kwa KO huku Parker akiwa na rekodi ya 24-0 akishinda 18 kwa KO na 6 kwa pointi.

Pambano litaanza majira saa 4:30 usiku kwa saa za Wales (Saa 6 usiku kwa saa za Afrika mashariki) na bingwa ataondoka na mikanda yote minne.