Njombe Mji FC yazidi kupokea kichapo

Kivumbi cha Ligi Kuu Bara kimeendelea tena jioni ya leo kwa viwanja vinne kuwaka moto.

Katika mchezo uliopigwa huko Shinyanga, wenyeji Stand United wametoa dozi ya mabao 3-1 dhidi ya Njombe Mji FC kutoka Njombe.

Mbao ya Stand United yamefungwa na Suleiman Ndikumana katika dakika ya kwanza ya mchezo huku mengine yakitiwa kimiani na Sixtus Sabilo kwenye dakika za 84 na 90. Bao pekee la Njombe Mji limefungwa na Notkelly Masasi katika dakika ya 75.

Wakati huohuo Kagera Sugar imelazimisha sare ya mabao 1-1 dhidi ya Ndanda FC katika dimba la Nangwanda Sijaona huko Mtwara, Ndanda wamejipatia bao lao kupitia Mrisho Ngassa (33') na Kagera wakijipatia goli kupitia Abdallah Mguhi ( 27').

Matokeo ya mechi zingine yalikuwa ni suluhu ya 0-0 kwa Mbeya City iliyoikaribisha Azam FC huko Mbeya, Sokoine Stadium. Ruvu Shooting nayo ikalazimishwa suluhu ya kutofungana na Tanzania Prisons Uwanja wa Mabatini.