Jeshi la Kenya lakamata wavuvi wa Kitanzania


Jeshi la wanamaji wa Kenya liliwakamata raia 109 wa Tanzania kwa kushiriki katika uvuvi haramu katika himaya ya maji ya Kenya katika bahari hindi.

Wavuvi hao walikamatwa katika eneo la Shimoni , linalomiliki bandari kusini mashariki mwa Kenya karibu na mpaka na taifa la Tanzania na kuwasilishwa mbele ya mahakama ya kaunti ya Kwale siku ya Jumatatu.

Wavuvi hao walizuiliwa baada ya kushindwa kulipa dhamana ya shilingi 20,000 za Kenya kila mmoja wao lilisema gazeti la Biashara nchini Kenya Business Daily , likimnukuu naibu wa kamishna wa Lungalunga Josphat Biwott.

Hatahivyo serikali ya Tanzania tayari imeanza harakati za kuhakikisha kuwa raia hao wanaachiliwa huru.

Naibu waziri wa uvuvi na ufugaji nchini Tanzania Abdalla Ulega ameliambia gazeti la The Citizen nchini humo kwamba juhudi zimeanza ili kuona kuwa tatizo hilo limetatuliwa.

''Tayari tumezungumza na wizara ya maswala ya kigeni na jeshi la polisi ili kuona vile tatizo hilo litakavyoangaziwa. Walikamatawa kulingana na sheria za Kenya'', alisema.

''Inapokuja katika uhalali wa vitendo vya uvuvi, kila taifa lina sheria zake ,Serikali inajua hilo'', alinukuliwa na gazeti hilo akisema