Serikali yajibu tukio la mwanamke kujifungulia Polisi


Kufuatia tukio la mwanamke mjamzito kujifungua kwenye Kituo cha Polisi Mang’ula mkoani Morogoro, serikali imebanwa bungeni na kutakiwa kutoa ufafanuzi.

Hoja hiyo iliibuliwa na Mbunge wa Meru, Joshua Nassari ambapo alitaka kujua kwa nini mwanamke huyo mjamzito aliyekuwa akikaribia kujifungua alikamatwa na kuwekwa mahabusu na baadaye uchungu kumbana akiwa nyuma ya nondo kabla ya baadaye kutolewa na kujifungua nje ya kituo hicho.

Akitoa ufafanuzi, Naibu Waziri wa Ndani, Hamad Masauni, amekiri kwamba busara haikutumika katika sakata hilo kwani chanzo cha kukamatwa kwake ni mali za wizi zilizonunuliwa na mumewe kukutwa ndani ya nyumba yake. Waziri Masauni ameeleza kwamba serikali inafuatilia kwa kina na wote waliohusika watachukuliwa hatua zinazostahili.