F Jeshi la Polisi lashiriki ujenzi wa makazi, latoa neno kwa wananchi | Muungwana BLOG
https://c2p.cleverwebserver.com/dashboard/6a0bec4b-79ba-11ef-ad2b-06f0639468d1

Jeshi la Polisi lashiriki ujenzi wa makazi, latoa neno kwa wananchi



Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya leo limeshiriki shughuli ya ujenzi na ukarabati wa nyumba za kuishi askari katika kambi ya Field Force Unit (FFU) Mbeya katika kuelekea maadhimisho ya miaka 57 ya uhuru wa Tanzania.

 Ukarabati huo umefanyika katika nyumba za kuishia askari ambazo zilikuwa katika hali mbaya (chakavu) na kuzirejesha katika hali nzuri. Sambamba na hilo, Jeshi la Polisi limeadhimia kujenga nyumba za kuishi askari katika kambi zake zilizopo maeneo mbalimbali.

 Aidha katika kuelekea maadhimisho hayo ya miaka 57 ya uhuru, licha ya kushiriki katika shughuli za ujenzi wa makazi ya askari, pia Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limeshiriki katika shughuli za usafi wa mazingira katika maeneo ya Mwanjelwa na Kabwe ikiwa ni hali ya kuhamasisha wananchi kushiriki usafi katika makazi yao na kuunga mkono jitihada za serikali za kuhamasisha usafi wa mazingira.

 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Ulrich Matei ametumia fursa hii nawaomba wana Mbeya kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuzuia uhalifu na kudhibiti ajali za barabarani kwa kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu na za madereva wasiotaka kutii sheria ili waweze kuchukuliwa hatua za kisheria mara moja.

 Aidha amewaomba wadau wenye mapenzi mema, kuunga mkono jitihada za Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya za ujenzi na ukarabati wa nyumba za kuishi askari unaoendelea katika kambi ya FFU Mbeya.