ATCL yazindua safari za Tanzania - Johannesburg Afrika Kusini


Shirika la ndege la Tanzania, (ATCL) limeanza Safari yake ya kwanza leo kuelekea Johannesburg nchini Afrika Kusini kwa kutumia ndege yake aina ya Airbus

Mkurugenzi wa Shirika hilo, Mhandisi Ladslaus Matindi amesema itakuwa inafanya Safari zake mara nne kwa wiki.

Ndege ya ATCL aina ya Airbus 220-300 imeondoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Salaam Tanzania (JNIA)  saa 4:30 asubuhi ikitarajia kutua katika Uwanja wa Kimataifa wa OR Tambo, Afrika Kusini saa 6:45 mchana.

Akizungumza na waandishi kabla ya ndege hiyo kuondoka leo Ijumaa, Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Elias Kwandikwa amesema lengo la kuanzishwa kwa safari hiyo ni kupunguza muda wa safari kwani abiria walikuwa wanaunganisha ndege ili kufika Afrika Kusini.

"Tupo tayari kuhudumia Watanzania na tutaendelea kufungua safari nyingi duniani," amesema Kwandikwa