Spika Tulia aingia mgahawani kupika, ahamasisha Mama lishe na wananchi kutumia nishati safi gesi


Na Mwandishi Wetu,Mbeya

SPIKA wa Bunge na Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini na Dkt. Tulia Ackson amehamasisha Mama lishe na wananchi kutumia nishati safi ya gesi  ili kutunza mazingira na kuokoa muda wa shughuli za kiuchumi huku akisisitiza kuwa umefika wakati wa kuachana na matumizi ya kuni na mkaa.

Dkt.Tulia amesema hayo  Septamba 30,2023  akiwa na wadau wa nishati safi ya kupikia kutoka Kampuni ya Gesi ya Oryx  baada ya kwenda katika Mgahawa uliopo Mtaa wa Uyole jijini Mbeya ambapo aliamua kupika chakula kwa gesi kwa ajili ya kuuza kwa wananchi kama sehemu ya kuonesha mfano kwa mama lishe na baba lishe kupika kwa gesi.

Akiwa katika mgahawa huo Dk.Tulia ambaye alipika chakula kwa kutumia jiko la Oryx amesema  lengo ni kuhamasisha watanzania kupikia nishati safi ikiwa ni kuunga mkono kampeni ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha wananchi wanatumia nishati safi badala ya mkaa na kuni.

Kwa upande wake Meneja wa Miradi ya Nishati Safi ya kupikia kutoka Kampuni ya Gesi ya Oryx Peter Ndomba amesema wamekuwa wakisaidia makundi mbalimbali yakiwemo ya Mama na Baba Lishe kupata nishati safi ya kupikia na tangu kwa kampeni ya kuhamasisha nishati safi wameshatoa mitungi ya gesi na majiko yake zaidi ya 70,000.

"Oryx tunafahamu dhamira ya Rais DK.Samia Suluhu ni kuhakikisha katika kipindi cha miaka 10 asilimia 80 ya Watanzania iwe inatumia nishati safi ya kupikia na Kampuni yetu imeibeba ajenda hiyo kwa vitendo.

"Leo hii tupo hapa tumeungana na Spika wa Bunge Dk.Tulia Ackson ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Mbeya kupitia taasisi ya Tulia Trust tuumekuwa naye katika jitihada hizi za nishati safi.Dk.Tulia ameamua kwenda moja kwa moja na amekuwa mfano na kielelezo cha matumizi ya nishati safi kwa wananchi,"amesema.

Amefafanua akiwa na Dk.Tulia wameshuhudia mama lishe wengi wanatumia kuni na mkaa,hivyo kuamua kwenda kwa mama Lishe na kupika kwa gesi maana yake ni kufikisha ujumbe kwa kundi kuona haja ya kutumia nishati safi ya kupikia.

"Dk.Tulia amekuwa mfano amepika mwenyewe kwa gesi na hii kwetu Oryx imetufurahisha  sana kupata kiongozi kama huyu ambaye amemua kuwa mfano wa moja kwa moja kwa wananchi. Ni alama kubwa sana kwamba hili jambo linawezekana...

"Watu wengi watabadilika, kwani tunafahamu makundi mbalimbali yakiwemo ya Baba na Mama Lishe ambao tunaona kila siku wako katika kuni na mkaa maisha yao yako hatarini.Tunaambiwa makundi yanayofanya shughuli za kupika yako hatarini zaidi.Watanzania zaidi ya 33000 wanafariki kila siku kwasababu ya kutumia kuni na mkaa .

"Mama Lishe na Baba Lishe maisha yao ni moto na kuni hivyo tukianza na kundi hili tunaweza kuokoa Watanzania ,kwa hiyo tunashukuru kwa Tulia Trust pamoja na vyombo vya habari kwa kupeleka taarifa kwa umma ili kila mmoja aifuate . Ndani ya wiki tatu zilizopita hapa Mbeya tumetoa mitungi ya gesi 1000 kwa mama Lishe na Baba Lishe."








 

Post a Comment

0 Comments