F Mamia wanufaika Kambi ya Madaktari bingwa Haydom. | Muungwana BLOG
https://c2p.cleverwebserver.com/dashboard/6a0bec4b-79ba-11ef-ad2b-06f0639468d1

Mamia wanufaika Kambi ya Madaktari bingwa Haydom.


Na John Walter -Mbulu
Katika kuelekea maadhimisho ya miaka 70 ya Hospitali ya Lutheran Haydom, kambi maalumu ya uchunguzi wa magonjwa imeanzishwa ili kusogeza huduma za kibingwa kwa wananchi wa Mkoa wa Manyara na maeneo ya jirani.

Kambi hiyo, inayofanywa na madaktari bingwa waliobobea katika magonjwa mbalimbali, imelenga kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya kwa wakati.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Lutheran Haydom, Daktari Bingwa wa Upasuaji, Dk. Daud Lotto, amesema kambi hiyo ni sehemu ya maadhimisho yatakayofanyika Machi 28 mwaka huu.

 "Lengo letu ni kutoa huduma za kibingwa kwa wananchi na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa uchunguzi wa afya mara kwa mara," alisema Dk. Lotto.

Zaidi ya wananchi 800 wamenufaika na huduma za uchunguzi na matibabu kupitia kambi hiyo, inayotolewa kwa ushirikiano kati ya Hospitali ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Mbulu, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Manyara na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Arusha.

Katika kambi hiyo, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Sikio, Pua na Koo, Dkt. Athanas Budadi kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara, amewataka wananchi kuacha tabia ya kujisafisha masikio kiholela, kwani inaweza kusababisha madhara makubwa. 

"Ni muhimu kufika hospitalini mara moja unapoanza kuhisi maumivu au tatizo lolote la masikio," alisisitiza.

Naye Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Kina Mama na Uzazi, Dkt. Colman Mayomba, amewahimiza wazazi kuhakikisha watoto wa kike wanapatiwa chanjo ya HPV ili kujikinga na saratani ya shingo ya kizazi. 

"Chanjo hii ni kinga madhubuti dhidi ya ugonjwa huu hatari, hivyo ni jukumu letu sote kuhakikisha watoto wetu wanapata huduma hii kwa wakati," alisema Dk. Mayomba.

Huduma Zilizotolewa

Kambi hiyo imetoa huduma mbalimbali za kibingwa, zikiwemo:

  • Magonjwa ya kina mama

  • Magonjwa ya watoto

  • Upasuaji mkubwa

  • Matatizo ya mfumo wa mkojo

  • Magonjwa ya macho

  • Magonjwa ya ndani

  • Matatizo ya mifupa

  • Magonjwa ya koo, masikio na pua

  • Uchunguzi wa mionzi

Baadhi ya wananchi waliopata matibabu wameeleza kuridhishwa na huduma hiyo, wakisema imewawezesha kupata matibabu bila kusafiri umbali mrefu.

"Tunamshukuru Mungu kwa kutufikisha miaka 70, karibu tukuhudumie!"

Aidha, wananchi wameshauriwa kupima afya zao mara kwa mara ili kugundua magonjwa mapema na kupata matibabu kwa wakati.


Post a Comment

0 Comments